6 Juni 2025 - 15:06
Waziri Mkuu wa Uingereza ametuma salamu za pongezi kwa Waislamu kwa mnasaba wa Sikukuu ya Eid al-Adha

Baadhi ya viongozi wa kisiasa wa Uingereza, wakiwemo Waziri Mkuu wa nchi hiyo, wametuma salamu za pongezi kwa Waislamu wa Uingereza na ulimwenguni kote kwa mnasaba wa Sikukuu ya Eid al-Adha.

Kwa mujibu wa Shirika la Habari la Ahlul-Bayt (a.s) –ABNA– Waziri Mkuu wa Uingereza, Keir Starmer, katika ujumbe aliouchapisha kwenye mtandao wa kijamii X, aliwapongeza Waislamu kwa mnasaba wa Sikukuu ya Eid al-Adha na kuandika:

“Eid al-Adha, ambayo huwadia mwishoni mwa ibada ya Hija, ni wakati muhimu wa sala na tafakari ya kina kwa Waislamu. Umuhimu wa Hija, kujitolea na umoja katika siku hii tukufu ni dhihirisho la kina cha huruma na ukarimu wa jamii ya Kiislamu kote duniani.”

Waziri Mkuu wa Uingereza, Keir Starmer, pia aliongeza:

“Katika siku hii, tunawakumbuka Waislamu walioko katika maeneo mbalimbali ya dunia ambao wanasherehekea Eid wakiwa katika hali ya migogoro, mateso au maumivu. Na iwe ni siku ambayo huimarisha mshikamano wa kijamii na kuleta matumaini mapya kwa wote.”

Meya wa Jiji la London, Sadiq Khan, naye katika ujumbe wake aliandika:

“Eid al-Adha ni fursa mahsusi ya kutafakari juu ya neema tulizonazo, kufufua upya ahadi ya imani, na kuonesha mshikamano na wale ambao wana hali duni zaidi. Eid al-Adha iwe ya baraka kwa wote.”

Chama cha Liberal Democrat, katika salamu zake, kilisema:

“Eid al-Adha iwe ya heri na baraka kwa wote wanaoisherehekea nchini Uingereza na duniani kote.”

Kiongozi wa chama hicho, Ed Davey, kupitia video aliyochapisha, alisema:

“Nawatakia Waislamu wote nchini Uingereza na kote ulimwenguni Eid yenye baraka, amani na furaha. Kwa wengi, huu ni wakati wa kuimarisha imani, familia na ukarimu – muda wa kuwa karibu na wapendwa na kujali hali ya wengine.”

Aliendelea kusema:

“Ninatambua kuwa siku hizi si rahisi, na wengi wenu mnabeba uzito wa yale yanayotokea hapa nyumbani na katika sehemu nyingine duniani. Kwa sababu hiyo, katika mwaka huu, nataka kueleza shukrani za pekee kwa Waislamu wa Uingereza ambao bado wanaendelea kujitokeza kwa ajili ya wengine, kuunga mkono jamii zao, na kuongoza kwa huruma na ujasiri. Nashukuru sana kwa yote mnayoyafanya.”

Viongozi wengine wa serikali na baadhi ya wabunge wa Uingereza pia walitoa salamu za pongezi kwa Waislamu kwa mnasaba wa sikukuu hii tukufu ya Kiislamu kupitia ujumbe wao binafsi.

Wakati huohuo, sala ya Eid al-Adha imefanyika leo (Ijumaa) kwa hamasa kubwa ya waumini Waislamu katika misikiti na vituo vya Kiislamu kote Uingereza. Aidha, jana – sambamba na Siku ya Arafah – wapenzi wa Nyumba Tukufu ya Allah nchini humo walikusanyika katika vituo vya Kiislamu, sambamba na mamilioni ya mahujaji walioko katika Jangwa la Arafah, kusoma dua tukufu na yenye maana ya Siku ya Arafah.

Tags

Your Comment

You are replying to: .
captcha